53:1Naapa kwa nyota inapo tua,
53:2Mwenzenu huyu hakupotea, wala hakukosea.
53:3Wala hatamki kwa matamanio.
53:4Hayakuwa haya ila ni ufunuo ulio funuliwa;
53:5Amemfundisha aliye mwingi wa nguvu,
53:6Mwenye kutua, akatulia,
53:7Naye yuko juu kabisa upeo wa macho.
53:8Kisha akakaribia na akateremka.
53:9Akawa ni kama baina ya mipinde miwili, au karibu zaidi.
53:10Akamfunulia mja wake (Mwenyezi Mungu) alicho mfunulia.
53:11Moyo haukusema uwongo uliyo yaona.
53:12Je! Mnabishana naye kwa aliyo yaona?
53:13Na akamwona mara nyingine,
53:14Penye Mkunazi wa mwisho.
53:15Karibu yake ndiyo ipo Bustani inayo kaliwa.
53:16Kilipo ufunika huo Mkunazi hicho kilicho ufunuika.
53:17Jicho halikuhangaika wala halikuruka mpaka.
53:18Kwa yakini aliona katika Ishara kubwa kabisa za Mola wake Mlezi.
53:19Je! Mmemuona Lata na Uzza?
53:20Na Manaat, mwingine wa tatu?
53:21Je! Nyinyi mnao wana wanaume na Yeye ndio awe na wanawake?
53:22Huo ni mgawanyo wa dhulma!
53:23Hayo hayakuwa ila ni majina mliyo wapa nyinyi na baba zenu. Mwenyezi Mungu hakuleta uthibitisho wowote juu ya hayo. Hawafuati ila dhana tu na kipendacho nafsi. Na kwa yakini uwongofu ulikwisha wafikia kutoka kwa Mola wao Mlezi.
53:24Ati mtu anakipata kila anacho kitamani?
53:25Mwenyezi Mungu tu ndiye Mwenye dunia na Akhera.
53:26Na wako Malaika wangapi mbinguni, ambao uombezi wao hautafaa chochote isipo kuwa baada ya Mwenyezi Mungu kutoa idhini kwa amtakaye na kumridhia.