73:20Hakika Mola wako Mlezi anajua ya kuwa hakika wewe unakesha karibu na thuluthi mbili za usiku, na nusu yake, na thuluthi yake. Na baadhi ya watu walio pamoja nawe kadhaalika. Na Mwenyezi Mungu ndiye anaye ukadiria usiku na mchana. Anajua kuwa hamwezi kuweka hisabu, basi amekusameheni. Basi someni kilicho chepesi katika Qur'ani. Anajua ya kuwa baadhi yenu watakuwa wagonjwa, na wengine wanasafiri katika ardhi wakitafuta fadhila ya Mwenyezi Mungu, na wengine wanapigana katika Njia ya Mwenyezi Mungu. Kwa hivyo someni kilicho chepesi humo, na mshike Sala, na toeni Zaka, na mkopesheni Mwenyezi Mungu mkopo mwema. Na kheri yoyote mnayo itanguliza kwa ajili ya nafsi zenu mtaikuta kwa Mwenyezi Mungu, imekuwa bora zaidi, na ina thawabu kubwa sana. Na mtakeni msamaha Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu.
74:1Ewe uliye jigubika!
74:2Simama uonye!
74:3Na Mola wako Mlezi mtukuze!
74:4Na nguo zako, zisafishe.
74:5Na yaliyo machafu yahame!
74:6Wala usitoe kwa kutaraji kuzidishiwa.
74:7Na kwa ajili ya Mola wako Mlezi, subiri!
74:8Basi litapo pulizwa barugumu,
74:9Siku hiyo, basi, itakuwa siku ngumu.
74:10Kwa makafiri haitakuwa nyepesi.
74:11Niache peke yangu na niliye muumba;
74:12Na nikamjaalia awe na mali mengi,
74:13Na wana wanao onekana,
74:14Na nikamtgenezea mambo vizuri kabisa.
74:15Kisha anatumai nimzidishie!
74:16Hasha! Kwani hakika yeye alikuwa akizifanyia inadi Aya zetu!
74:17Nitamtesa kwa mateso yasio wezekana.
74:18Kwani hakika yeye alifikiri na akapima.