80:41Giza totoro litazifunika,
80:42Hao ndio makafiri watenda maovu.
81:1Jua litakapo kunjwa,
81:2Na nyota zikazimwa,
81:3Na milima ikaondolewa,
81:4Na ngamia wenye mimba pevu watakapo achwa wasishughulikiwe,
81:5Na wanyama wa mwituni wakakusanywa,
81:6Na bahari zikawaka moto,
81:7Na nafsi zikaunganishwa,
81:8Na msichana aliye zikwa hai atapo ulizwa,
81:9Kwa kosa gani aliuliwa?
81:10Na madaftari yatakapo enezwa,
81:11Na mbingu itapo tanduliwa,
81:12Na Jahannamu itapo chochewa,
81:13Na Pepo ikasogezwa,
81:14Kila nafsi itajua ilicho kihudhurisha.
81:15Naapa kwa nyota zinapo rejea nyuma,
81:16Zinazo kwenda, kisha zikajificha,
81:17Na kwa usiku unapo pungua,
81:18Na kwa asubuhi inapo pambazuka,
81:19Kwamba hakika bila ya shaka hii ni kauli ya Mjumbe mtukufu,
81:20Mwenye nguvu na mwenye cheo kwa huyo Mwenye Kiti cha Enzi,
81:21Anaye t'iiwa, tena muaminifu.
81:22Na wala huyu mwenzenu hana wazimu.
81:23Na hakika yeye alimwona kwenye upeo wa macho ulio safi.
81:24Wala yeye si bakhili kwa mambo ya ghaibu.
81:25Wala hii si kauli ya Shetani maluuni.
81:26Basi mnakwenda wapi?
81:27Haikuwa hii ila ni ukumbusho kwa walimwengu wote.
81:28Kwa yule miongoni mwenu anaye taka kwenda sawa.
81:29Wala nyinyi hamtataka isipo kuwa atake Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa walimwengu wote.